MV Magogoni yaanza kufanyiwa ukarabati


Ukarabati mkubwa wa kivuko cha MV Magogoni umeanza rasmi mara baada ya kusitisha huduma zake hivi karibuni.

Akizungumza mara baada ya kutembelea eneo la bandari kujionea kazi ya ukarabati kwa kivuko hicho, Kaimu Mtendaji Mkuu TEMESA Mhandisi Manase Ole-kujan amesema kazi ya ukarabati wa kivuko hicho umeanza kwa hatua za awali za kukifanyia usafi ili kuona maeneo yaliyoharibika na kuyafanyia ukarabati.

“Muda wake wa matengenezo umefika na ni wakati muafaka kwa kivuko kufanyiwa matengenezo ni muda mrefu kimehudumia wananchi wa Jiji la Dar es Salaam lakini mara baada ya kukamilika kwa ukarabati wake kitarudi kutoa huduma kama kawaida,” alisema Mhandisi Manase.

Mhandisi Manase ameongeza kuwa ukarabati huo utazingatia viwango vya kimataifa ili kukiwezesha kivuko hicho kudumu kwa muda mrefu bila ya kupatwa na hitilafu yoyote ya kiufundi na kuwaasa wahandisi husika kufanya ukarabati huo na kukamilika kwa muda uliopangwa.

Aidha Mhandisi Mkuu Kutoka kampuni ya Songoro Marine Boat yard LTD Major Songoro amesema kwa kushirikiana na waandisi kutoka TEMESA watahakikisha wanamaliza kazi ya ukarabati kwa wakati na kwa ufanisi wa hali juu ili kurejesha huduma ya Kivuko hicho.

Kivuko cha MV Magogoni kinachotoa huduma eneo la Magogoni na Kigamboni Jijini Dar es Salaam kimesitisha kutoa huduma kwa ajili ya kufanyiwa matengenezo makubwa na kwa sasa kivuko cha MV Kigamboni kinashirikiana na MV. Lami kutoa huduma kwa wananchi.

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top