Uamuzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) juu ya adhabu ya kadi nyekundu aliyooneshwa nahodha wa Simba, Jonas Mkude

Mkude huru Simba



Jonas Mkude
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limefuta adhabu ya kadi nyekundu aliyooneshwa nahodha wa Simba, Jonas Mkude katika mechi ya timu hiyo dhidi ya Yanga iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam
mwishoni mwa wiki iliyopita.

Kama angekutwa na hatia na kadi hiyo kubaki, Mkude angekosa mechi tatu na kamati ingemhukumu kifungo cha kuanzia miezi mitatu adhabu ambayo hupewa mchezaji aliyeoneshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja na kumshambulia mtu ambaye hakuwa na mpira.

Kuondolewa kwa adhabu hiyo kumemwepusha Mkude na kifungo cha kukosa mechi tatu, na adhabu ya kufungiwa si chini ya miezi mitatu.

Hiyo ni kutokana na aina ya kosa hilo kwamba mbali na kufuta kadi hiyo, kamati ya bodi ya ligi ya uendeshaji na usimamizi wa ligi imewaweka kiporo waamuzi wawili wa mechi hiyo Martin Saanya (katikati) na Samwel Mpenzu (pembeni) wakichunguzwa kuhusu uchezeshaji wao wa mechi hiyo.

Mechi hiyo iliyoisha kwa sare ya bao 1-1 ilitawaliwa na vurugu iliyosababisha kuharibika kwa miundombinu ya Uwanja wa Taifa, ikiwa ni pamoja na kuvunjwa mageti na kung’olewa viti.

Mwamuzi wa mechi hiyo, Martin Saanya alimwonesha Mkude kadi nyekundu ikidaiwa kuwa nahodha huyo alimpiga baada ya kukubali bao la kuongoza la Yanga lililofungwa na Amisi Tambwe ambaye kabla ya kufanya hivyo alishika mpira na mkono na ndipo kilipozuka kizaazaa.

Lakini taarifa ya TFF kwa vyombo vya habari jana ilisema kamati ya bodi ya ligi ya uendeshaji na usimamizi wa ligi iliyokutana juzi iliifuta adhabu hiyo ya Mkude baada ya kuthibitika pasi na shaka kuwa nahodha huyo hakustahili adhabu hiyo.

“Mbali na ripoti ya kamishna na kupitia tena mkanda wa mechi hiyo iliyooneshwa ‘live’ kama inaendelea na uchunguzi wa jambo lingine kuhusu uchezeshaji wa mwamuzi wa mechi hiyo Martin Saanya na wasaidizi wake Samwel Mpenzu na Ferdinand Chacha kabla ya kutangaza uamuzi wake,” ilisema taarifa hiyo.

Hata hivyo habari za uhakika zilizopatikana juzi kutoka ndani ya kikao hicho zilidai kamati iliwafungia miaka miwili Saanya na Mpenzu. Aidha, kamati hiyo imeipiga faini ya Sh milioni tano klabu ya Simba kwa kitendo cha mashabiki wake kung’oa viti katika mechi hiyo na kuiagiza ilipe gharama za uharibifu zilizofanywa siku hiyo.

“Kamati hiyo katika kikao chake imekilaani kitendo hicho na kuionya klabu hiyo kuwa vitendo vya aina hiyo vikiendelea itakabiliwa na adhabu kali ikiwemo kucheza bila mashabiki, adhabu hii ya Simba imetolewa kwa mujibu wa kanuni ya 42(3) na 24(7) za Ligi Kuu,” ilisema taarifa hiyo.. Mwingine aliyepitiwa na ‘rungu’ la adhabu katika mechi hiyo ni Ofisa habari wa Simba Haji Manara aliyetozwa faini ya Sh 200,000 kwa kitendo chake cha kuingia uwanjani baada ya mechi hiyo wakati yeye hakuwa miongoni mwa maofisa wa mechi waliotakiwa kuingia katika eneo hilo.

Aidha, Azam imepigwa faini ya Sh milioni tatu kwa kuvaa nembo ya mdhamini wa Ligi Kuu mkono mmoja badala ya miwili, jambo ambalo ni kinyume na kanuni ya 13 (1) na adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa kanuni ya 13 (6).

Nayo JKT Ruvu imepewa onyo na kutozwa faini ya Sh 500,000 baada ya msimamizi wa kituo na ofisa wa bodi ya ligi kushambuliwa na mashabiki wa timu hiyo katika mechi dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi, Pwani.

Shabiki huyo amefungiwa miezi 12 na iwapo vitendo hivyo vitaendelea uwanja huo utafungiwa kutumika kwa mechi za Ligi Kuu.

Aidha Mwamuzi Ahmed Seif amefungiwa miezi sita kwa kushindwa kumudu mechi ya African Lyon dhidi ya Mbao FC, ikiwemo kutoa penalti isiyostahili. Mwamuzi huyo pia alipata alama za chini ambazo hazikumruhusu kucheza Ligi Kuu.

“Pia makamisaa David Lugenge na Godbless Kimaro wamepewa onyo kwa kuwasilisha taarifa zenye upungufu katika mechi za raundi ya tano na saba walizozisimamia,” ilisomeka taraifa hiyo. 


Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top