MARK CLATTENBURG MWAMUZI ALIYEPITA MLANGO WA NYUMA KUCHEZESHA FAINALI YA EURO 2016 URENO V UFARANSA

Mark Clattenburg ndiye mwamuzi atakaekuwa mwamuzi wa mchezo wa fainali ya Euro 2016 kati ya Ureno na Ufaransa, inawezekana kuna kitu kimaja watu wengi hawakifahamu kuhusu mwamuzi huyu raia wa England.

Kamati ya waamuzi wa Uefa ambayo mwenyekiti wake ni mwamuzi wa zamani wa Italia aliyepata umaarufu mkubwa enzi zake wakati anapuliza filimbi mzee kipara Pierluigi Collina, anamkubalia sana Mark Clattenburg.

Kwenye michakato hii ya kupata waamuzi wa kuchezesha michuano ya Euro, Uefa walichokifanya kupitia kamati ya akina Collina, waliwaambia wanachama wao kwa maana nchi wanachama wa Uefa kila nchi iteue jina la mwamuzi ambaye wao kama nchi wanamuona ndiyo bora halafu majina hayo wao watayapokea.

Kwahiyo yakapendekezwa majina 53 kwa maana kila nchi iliteua jina moja na wao kama kamati wakakaa chini na kuanza kupitia majina yote na mwisho wa siku yakabaki majina 18.

Sasa hii hapa ndiyo story ya Mark Clattenburg kuingia Euro 2016

Kwenye jina lililoteuliwa na FA, huwezi amini jina la Clattenburg halikuwepo. Aliyeteuliwa kama mwamuzi bora wa England alikuwa ni Martin Atkinson ambaye ndiye jina lake lilipelekwa Uefa kama mwamuzi bora kutoka England.

Lakini Uefa walipokaa na kamati yao ya waamuzi chini ya Collina wakati wanachuja kupata cream ya waamuzi 18, wakagundua jina la Mark Clattenburg halipo, walichokifanya kwasababu Martin Atkinson tayari alishapitishwa na FA, ilibidi wamteue Clattenburg kama kamati ya waamuzi na hasa Collina, yeye binafsi alisema kabisa mwamuzi anayemkubali ni Clattenburg.

Kupitia mlango wa nyuma, Clattenburg akateuliwa kuwa miongoni mwa waamuzi 18 watakaochezesha fainali za Euro 2016. Kila nchi ilitoa mwamuzi mmoja lakini England pekeyake ikatoa waamuzi wawili kati ya 18. Mwamuzi wa pili ni kwasbabu ya pendekezo maalum la kamati ya waamuzi wa Uefa.

Mark Clattenburg akachezesha mechi ya Italia na Ubelgiji akachezesha mechi nyingine kati ya Jamhuri ya Czech dhidi ya Croatia, hapa ndipo huyu jamaa anapojikusanyia sifa. Namana anavyosimamia mchezo ni tofauti na waamuzi wengine wengi. Nikukumbushe tu mechi ya fainali ya Uefa Champions League pale Milan, Pepe ambaye alifanya vurugu nyingi kwenye mchezo ule kwa kujiangusha na kutaka kuwatengenezea makosa wenzake.

Baada ya Clattenburg kugundua kama Pepe anafanya mchezo mbaya angekuwa mwamuzi mwingine, angemwadhibu Pepe kwa kumpa kadi lakini kwa kujua ukubwa na umuhimu wa mechi ya fainali, alichokifanya yeye kama mwamuzi ni kwenda kwa Pepe na kumpa ‘makavu live’ kwa kile alichokuwa anakifanya, Pepe hakufanya tena ujinga wake aliokuwa anaufanya awali.

Kwahiyo utaona jukumu la mwamuzi siyo tu kumwadhibu mchezaji anapokosea, lakini ni jukumu lake kuulinda mchezo na kuubeba kutokana na ukubwa wake ili umalizike salama.

Kwenye mechi ya Euro kati ya Jamhuri ya Czech na Croatia ilikuwa na vurugu nyingi ikiwemo mashabiki kurusha mafataki uwanjani, wachezaji wa timu zote mbili walikuwa wakipambana na wakati mwingine kutaka kupigana wakati huo mshambuliaji wa Croatia Mario Mandzukic aliwafata mashabiki wa Czech na kuwabugudhi lakini mwamuzi alichokifanya, alimfata Mandzukic akamwambia hii shughuli ya kutoa mafataki uwanjani si yako, wewe ni mchezaji hutakiwi kufanya vurugu, akamvuta na kumsogeza pembeni na Mario Mandzukic akaendelea na mambo yake.

Hivyo ni baadhi ya vitu ambavyo vinampa heshima na sifa zingine za ziada, kwahiyo inapotokea nafasi kama hii wanakaa kamati ya waamuzi kwa kuangalia ukubwa wa mchezo ambao unasubiriwa na mamilioni ya watu duniani zaidi ya watu milioni 300 wanasubiri kuitazama mechi hii basi kuna vitu vingine vya ziada ambavyo wanaviangalia na kumpa mtu imara ambaye anaweza kumudu mechi husika.

Kuna kitu kingine ambacho watu wengi hawajui, anapopatikana mwamuzi wa kati wa kuchezesha mechi, wasaidizi wake pia inabidi watoke nchi mmoja na mwamuzi wa kati ili kuweza kutengeneza mazingira rafiki ya mawasiliano.

Wasaidizi wa Clattenburg wanatoka England, kwenye orodha ya wasaidizi kuna orodha yenye majina ya Simon Beck na Jake Collin ambao watashika vibendera. Lakini kwenye michuano hii ya Euro utaona kuna waamuzi wanaokaa nyuma ya magoli, nyuma ya goli moja atakaa Anthony Taylor na nyuma ya goli jingine atakaa Andre Marriner ni waingereza pia.

Kwenye mechi zote kubwa za Uefa, Anthony Taylor amekuwa msaidizi na hii ni kutokana na umahiri mkubwa aliokuwa nao. Kwahiyo inawezekana pia kwasababu Uefa ilitaka kuwatumia hawa waamuzi ambao inawaamini ambao ni wasaidizi, wakaamua kutafuta mwamuzi wa kukaa kati ambaye anatoka kwenye nchi moja na hawa na hapo ndipo jina la Clutternburg likaingia.
Credit:Shaffi

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top