AUDIO: Askari polisi 6 wa Kikosi cha Usalama Barabarani Watumbuliwa



Askari polisi sita wa Kikosi cha Usalama Barabarani, wameondolewa baada ya kukiuka taratibu za kazi.


Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamishana Msaidizi Mwandamizi wa Polisi
ambaye pia ni Mkuu wa Operesheni, Kitengo cha Usalama Barabarani Tanzania, Fortunatus Musilimu, alisema askari hao watapangiwa kazi nyingine.


Kwa mujibu wa Kamishna Musilimu, askari hao kutoka katika mikoa mbalimbali nchini, waliondolewa wakati wa ukaguzi wa utendaji wa kazi kwa askari wa kikosi hicho.


“Ukaguzi huo ulifanyika nchi nzima katika barabara kuu kufuatia mpango mkakati wa kupunguza ajali za barabarani nchini,” alisema kiongozi huyo wa polisi.


Aliwataja askari hao kuwa ni D 9363 Sajenti Richard aliyekuwa wilayani Misungwi, Mkoa wa Mwanza, G 9958 PC, Edward, aliyekuwa eneo la Lilambo mkoani Ruvuma, H 8234 PC Mungwe, aliyekuwa eneo la Tanesco Jimboni, wilayani Mbinga, Mkoa wa Ruvuma na WP 3058 Koplo Mariam, aliyekuwa eneo la Igurusi, Mbeya.


“Askari hao walikutwa wakiwa hawakuvaa namba za Jeshi la Polisi kama utambulisho wao kazini, kitendo ambacho ni utovu wa nidhamu na kutozingatia maadili ya kijeshi.


“Yaani kitendo cha kutovaa namba kiliashiria askari hao walikuwa wababaishaji, walikuwa wakificha maovu, hawakuwa wawazi katika utendaji kazi wao na pia waliashiria kujihusisha na vitendo vya rushwa.


“Mbali na hao, askari wengine waliochukuliwa hatua ni D 9603, Sajenti Samwel na G 8264, PC Dickson, waliokutwa eneo la Hanihani, wilayani Igunga, Mkoa wa Tabora.


“Hawa walikutwa katika mazingira yanayoonyesha walikuwa wakijihusisha na vitendo vya waziwazi vya kudai rushwa kutoka kwa wenye magari yaliyokuwa na makosa,” alisema Kamishna Musilimu.


Kutokana na hali hiyo, aliwataka askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani kufanya kazi kwa uadilifu ili wasichukuliwe hatua.


==>Msikilize hapa Kamanda Muslimu akifafanua sababu za uamuzi huo:- 

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top