Jaribio la Mapinduzi Uturuki lafanyika usiku wa kuamkia leo, Rais Erdogan ajitokeza Istanbul



Kundi la wanajeshi lilitangaza mapinduzi kupitia runinga ya taifa

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amejitokeza katika uwanja wa ndege wa Istanbul, akiwa amezingirwa na mamia ya wafuasi baada ya kundi la
wanajeshi kujaribu kupindua serikali yake.

Kwenye kikao cha dharura na wanahabari, ameahidi kusafisha jeshi na akaahidi kwamba wote waliohusika wataadhibiwa vikali.

Kundi la wanajeshi lilikuwa limetekeleza jaribio la kupindua serikali.

Taarifa kutoka kwa kundi hilo la jeshi, ambayo ilisomwa kupitia runinga ya taifa ilisema jeshi lilikuwa limechukua mamlaka. Raia walijitokeza barabarani kumuunga mkono Bw Erdogan

Hata hivyo, Waziri Mkuu wa Uturuki Binali Yildirim ameambia runinga moja ya Uturuki kwamba hali imethibitiwa na kwamba waliohusika wataadhibiwa vikali.

Mashirika ya haabri ya serikali yanaripoti kuwa majengo ya bunge mjini Ankara yamekumbwa na mlipuko wa bomu.

Kituo cha runinga cha kibinafsi cha NTV kinasema ndege ya kivita ya wanajeshi watiifu kwa serikali imeidungua helikopta iliyokuwa ikitumiwa na wanajeshi waliotekeleza jaribio la mapinduzi mjini Ankara.

Milio ya risasi inasikika katika moja ya madaraja makubwa zaidi kwenye mto Bosphorus, katika mji mkubwa zaidi Uturuki, Istanbul. Makabiliano yanadaiwa kuwa kati ya wanajeshi na waandamanaji.

Wakati wa kutangaza mapinduzi ya serikali, kundi hilo la wanajeshi lilisema lilichukua hatua hiyo kuhifadhi utawala wa demokrasia na likatangaza amri ya kutotoka nje.

Lilisema nchi hiyo ingeongozwa na “baraza la amani” ambalo lingehakikisha utulivu na usalama.

Aidha, liliahidi kwamba utawala wa kikatiba ungerejeshwa “haraka iwezekanavyo”.



Jaribio hilo la mapinduzi ya serikali lilitekelezwa Rais Erdogan akiwa likizoni.

Alihojiwa baadaye kwenye runinga, kupitia simu na mtandao wa Facetime, ambapo alitoa wito kwa watu kujitokeza barabarani kuunga mkono demokrasia.


Alisema jaribio hilo la mapinduzi lilitekelezwa na kundi la wachache jeshini.

Marekani, Urusi, NATO na Umoja wa Ulaya wote wamehimiza kuwepo kwa utulivu na uthabiti.

Waziri wa mambo ya nje ya Marekani John Kerry amesisitiza kwamba Marekani itaunga mkono serikali ya Uturuki iliyochaguliwa kidemokrasia pamoja na taasisi zake.

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top