CUF yatoa tamko,Yamtaka Prof Lipumba asikivuruge Chama

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.

KAULI TATA YA PROFESA LIPUMBA KUHUSU KURUDI KATIKA NAFASI UENYEKITI WA TAIFA WA CHAMA CHA WANANCHI CUF.

(Imetolewa na Kamati ya Uongozi ya CUF ambayo imepewa dhamana la Kuongoza chama kutoka kwa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa, Tarehe 17 June 2016)

Waheshimiwa Waandishi wa habari, kwa niaba ya Chama Cha Wananchi CUF napenda kuwakaribisha katika ukumbi wa mikutano wa Shaabani Khamis Mloo hapa Buguruni Dar es salaam.

Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa dhati kabisa wanahabari wote na vyombo vya habari kwa ujumla kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kuwahabarisha wanajamii juu ya yale yanayoendelea katika nchi na hata taarifa za nje ya mipaka ya nchi yetu. Kwa muktadha huo, natarajia pia katika tukio la leo, wananchi kupitia vyombo vyenu watapata fursa nyingine ya kufahamu nini kama Chama tunawajulisha.

Juni 13, 2016 Profesa Ibrahim Lipumba aliitisha kikao na Waandishi wa habari katika ukumbi wa Shaaban Khamis Mloo akiwa amekieleza Chama kwamba anadhamiria katika kikao hicho kufanya uchambuzi wa Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Waziri wa fedha Mhe, Philip Mpamgo kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa na Bunge kwa mwaka wa fedha wa 2016 – 2017.

Ni jambo la kawaida kwa Profesa Lipumba kuomba kufanya kikao na waandishi wa habari akitumia ukumbi wa Chama na kuzungumzia masuala mbalimbali yakiwemo ya kisiasa na wakati mweingine hata masuala ya kitaaluma ambayo yanamaslahi ya moja kwa moja na wananchi wa Tanzania na jamii kwa ujumla. 

Uamuzi wa kumruhusu Profesa Lipumba kutumia ukumbi wa Chama umefikiwa kwa kuzingatia ukweli kwamba yeye ni mmoja ya wanachama ambao wamekitumikia Chama hiki kwa kipindi kirefu na kwa mafanikio makubwa.

Hivyo pamoja na kwamba aliamua kwa hiyari yake mwenyewe kujiuzulu nafasi ya Uenyekiti wa taifa mnamo August 5, 2015 kwa kumwandikia barua Katibu Mkuu akimtaarifu juu ya uwamuzi wake huo, Chama kiliona busara ya kumuenzi kwa kumpatia heshima kwa fursa ya kutumia mali za chama kutokana na mchango wake ambao wakati wote amekuwa akikipatia chama na kwa kuzingatia kuwa majukumu ambayo mara nyingi amekuwa anayafanya na ambayo hulazimika kuzungumza na vyombo vya habari, sehemu kubwa yana maslahi kwa Chama.

Waheshimiwa wanahabari, tumelazimika kuitisha kikao hiki leo ili kupata fursa ya kutoa ufafanuzi wa masuala kadhaa ambayo wanachama wetu katika ngazi mbalimbali wamekuwa wanahangaika kutokana na kauli ya Profesa Lipumba ya tarehe 13 Juni 2016 kwamba amemwandikia barua Katibu Mkuu wa Chama Maalim Seif Sharif Hamad ya kurudi katika nafasi yake ya Uwenyekiti wa Chama taifa.

Katika taarifa yake aliyoitoa kwa waandishi wa habari Profesa Lipumba alisema kwenye ukurasa wa tatu aya ya tano na nakuu “Kwa kuzingatia changamoto za kisiasa zinazoikabili nchi yetu na Chama chetu nimekubali rai ya viongozi wa dini, wanachama na baadhi ya viongozi nirejee kwenye uongozi wa Chama. Kwa kuwa barua yangu ya tarehe 5 Agosti 2015 ilikuwa haijajibiwa, nimemuandikia barua Katibu Mkuu kuitengua barua yangu ya kujiuzulu na kurejea kwenye nafasi yangu niliyochaguliwa ya Mwenyekiti wa Taifa” mwisho wa kunukuu.

Waheshimiwa waandishi wa habari; yapo maswali kadhaa ambayo wanachama wanatuuliza ambayo kimsingi yanahitaji majibu ya msingi:

Mosi wanachama wanataka kujua nini hasa sababu ya msingi iliyosababisha Profesa Lipumba aamue kujiuzulu nafasi ya uongozi mpaka akaandika barua ya kung’atuka uongozi Agosti 5, 2015?

Je sababu hizo kwa sasa zimetafutiwa ufumbuzi wake na kwamba haziwezi kutokea tena?

Ikiwa sababu hizo hazipo kwa sasa, zikijitokeza tena atachukua uwamuzi uleule wa kujiuzulu?

Iweje Profesa Lipumba akae nje ya uongozi kwa takribani miezi kumi ndiyo leo aamue kuandika barua ya kufuta barua ya awali ya kujiuzulu?

Hivi madai ya kutojibiwa barua yake ya tarehe 5 Agosti aliyompelekea Katibu Mkuu, ndiyo msingi wa hoja yake ya kurudi katika nafasi ya uwenyekiti, hajui kwamba Mkutano Mkuu wa taifa haukuhitajika kufanyika kwa ajili ya jambo hili?

Hivi wale wajumbe walioteuliwa na Baraza Kuu la uongozi la taifa kuunda Kamati ya Uongozi wanaenda wapi sasa baada ya yeye kuamua kujirudishia uongozi?

Hivi yeye Lipumba na Baraza Kuu nani Mkubwa kimamlaka mpaka afikie hatua kutoheshimu uwamuzi wa Baraza?

Lipumba hasa kwa uamuzi wake wa kujirudishia uenyekiti wa taifa ametumia kipengele kipi cha Katiba ya Chama hasa baada ya kuvitaja vipengele kadhaa ya Katiba katika Ibara ya 117?

Kimsingi maswali haya tumeshindwa kuyajibu kwa ufasaha. Chama cha Wananchi CUF kinapenda kuchukua nafasi hii kumuomba Profesa Lipumba kwamba asijaribu kukiyumbisha Chama katika kipindi hiki ambacho nchi ina matatizo makubwa ambapo Watanzania wanahitaji kuwekwa pamoja na kupewa matumaini ya namna gani matatizo yao yanaweza kutatuliwa.

Kinyume chake, wapo wananchi wengi wanaweza kujengwa na fikra kwamba hatua ya baadhi ya wanaojiita wafia Chama wa CUF ambao nyakati zote wamekuwa wanapita katika maeneo mbalimbali kutoa kauli za uongo kwa lengo la kuwagawa viongozi wa Chama na wanachama wake ambapo kimsingi imebainika kwamba hawa wanatumiwa na Maadui wa Chama hiki (CUF) kwa lengo la kukidhoofisha, inaweza kuonekana kwamba yana Baraka yake na hivyo kushusha heshima yake kwa jamii.

CUF kinapenda kuwahakikishia wanachama wote na jamii kwa ujumla kwamba bado kipo Imara, na kwamba tutahakikisha Katiba yetu ya Chama na Kanuni zake zinazingatiwa wakati wote na kwamba kila mwanachama atapata haki yake kwa mujibu wa Katiba yetu, hakuna atakayedhulumiwa.

Tunawaomba wanachama, wapenzi na Watanzania kwa ujumla wawe watulivu katika kipindi hiki wakati taratibu zikichukuliwa na viongozi wetu kwa kutafakari yanayojiri kila wakati na kwamba tunawahakikishia Chama kina viongozi madhubuti wanaojua Chama kimetoka wapi, tupo wapi na tunataka kwenda wapi. Maamuzi ya Chama hayatalenga kumwonea mtu wala kumwonea haya bali yatalenga kutoa haki ambayo kila mmoja atastahili kuipata.

Aidha tunapenda kuwahakikishia na kuwaomba wajumbe wa Mkutano Mkuu wa taifa kwamba mkutano bado upo palepale kama ulivyopangwa na Kamati ya Utendaji ya taifa baada ya kuidhinishwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa ambapo imapitishwa kwamba Mkutano Mkuu wa taifa utafanyika tarehe 21 August 2016 katika Ukumbi wa Hoteli ya Landmark iliyopo Ubungo jijini Dar es salaam.

Wajumbe wa Mkutano Mkuu wajiandae kuja kufanya mamuzi yatakayopelekea kukiimarisha Chama kwa kujaza nafasi za uongozi zilizo wazi katika ngazi ya taifa.

Utulivu wa wanachama, wapenzi wetu na Watanzania kwa ujumla wenye maslahi na Chama Hiki kwa wakati huu ni muhimu zaidi pengine kuliko wakati mwingine wowote ambao umeweza kutokea na kwamba tutambue kuwa CUF ni Chama Imara chenye Uongozi Madhubuti, Nuru ya Matumaini hivyo ni jukumu la wanachama kuanza kuchunguzana kuona ikiwa wote tunaimba wimbo mmoja au wapo wanaotaka kutuimbisha nyimbo tofauti kwa malengo yaliyojificha, tuwe nao makini ili wajibainishe.

Imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi Taifa,
Twaha Issa Taslima.
MUNGU IBARIKI CUF, MUNGU IBARIKI TANZANIA.
Habari Kuu leo Bofya hapa
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top