SERIKALI IMEZITAKA TAASISI ZAKE KUFUATA SHERIA YA MANUNUZI YA UMMA YA MWAKA 2011


Wakili wa Serikali Mwandamizi, Benno Sanga akifafanua kuhusu matumizi ya sheria ya manunuzi ya umma na umuhimu wake leo Jijini Dodoma.


Baadhi ya Mawakili wa Serikali waliohudhuria semina hiyo wakisikiliza kwa makini mafunzo hayo yaliyofanyika leo Mjini Dodoma.

Serikali imezitaka taasisi zake zote kufuata sheria ya<Endelea bofya kichwa cha habari hii juu>

Hayo yamesemwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Benno Sanga kwenye Mafunzo ya Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2011 kwa Mawakili wote nchini iliyofanyika mjini Dodoma.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yamelenga kuwapa mawakili ujuzi katika utoaji mzuri wa ushauri wa kisheria kwa Taasisi za Serikali.

Wakili Mwandamizi Sanga alisema kuwa msingi mkubwa wa sheria hiyo ni ushindanishwaji wa wazabuni unaoweza kuiletea Serikali thamani ya fedha.

“Kila taasisi ya serikali lazima ifuate sheria ya manunuzi kwa manunuzi mbalimbali ya vifaa vya ofisi,sheria hii imeweka utaratibu wa kuhakikisha fedha iliyotumiwa inalingana na huduma inayopatikana”,alisema Sanga

Akitoa mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Mikataba (Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali) Bi.Monica Otaru alisema mafunzo hayo yatawasaidia mawakili kufanya upekuzi wa mikataba kwa makini na uhakika zaidi.

“Pamoja na kuwa kazi ya kupekua mikataba ni sehemu ndogo ya kazi zetu lakini inachukua muda mwingi, hivyo mafunzo haya yatawaandaa Mawakili wa Serikali walioko katika Ofisi za Kanda kuweza kufanya upekuzi wa mikataba kwa umakini na uhakika zaidi”,alisema Bi. Otaru.

Aidha, Bi. Otaru amezitaja baadhi ya changamoto zinazosababisha kazi ya uhakiki wa mikataba kutofanyika kwa usahihi zikiwemo za mikataba kukosa maelezo na maoni kamili ya taasisi husika.

Alitaja changamoto nyingine kuwa ni gharama za kusafirisha mikataba kutoka taasisi husika,ugumu wa njia za mawasiliano pamoja na kutoshirikishwa kwa taasisi husika katika mchakato wa manunuzi na uandaaji wa mikataba.

Naye Wakili wa Serikali Mwandamizi Divisheni ya Mikataba, Said Kalunde ameelezea juu ya mambo muhimu ya kuzingatia katika kufanya upekuzi wa mikataba ya ununuzi ikiwemo ujazaji wa fomu mbalimbali zinazotumika katika uhakiki wa mikataba kwa mujibu wa Sheria hiyo ya manunuzi.

“Ni muhimu sana kwa wakili kujiridhisha kama taratibu za ujazaji wa fomu zimefuatwa na fomu zimejazwa kwa usahihi,endapo wakili hatojiridhisha kwa kuhakiki fomu hizo huenda akapatwa na matatizo makubwa ya kiutendaji”,alisema Kalunde.

Mafunzo hayo yametolewa kwa mawakili wa serikali divisheni ya mikataba ili kuwajengea uwezo wa kutekeleza jukumu la kuhakiki mikataba inayotokana na wazabuni.

Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeundwa chini ya kifungu cha 59 cha Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni mshauri wa masuala ya kisheria kwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya kifungu cha 59(3) cha Katiba ya mwaka 1977

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top