Serikali Yasema Waliosoma shahada za sayansi Watapewa Mafunzo ya Muda Mfupi ya Ualimu ili Kukabiliana na Tatizo la Upungufu wa Walimu

Na Beatrice Lyimo-MAELEZO, Dodoma


Serikali imeanza kupanga walimu wa sayansi moja kwa moja katika shule badala ya Halmashauri kama ilivyokuwa awali ili kuleta uwiano sawa wa walimu katika shule mbalimbali nchini.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Suleman Jaffo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Muleba Prof. Anna Tibaijuka lililohusu mkakati wa Serikali katika kukabiliana na tatizo la upungufu wa walimu.

Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa Serikali imeandaa mkakati wa kuwaajiri wahitimu wa shahada za sayansi ambazo siyo za ualimu baada ya kuwapa mafunzo ya muda mfupi kuhusu mbinu za ufundishaji na maadili ya ualimu ili kukabiliana na changamoto ya walimu wa sayansi nchini.

Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa tayari kibali kimeombwa katika Ofisi ya Rais Utumishi kwa ajili ya utekelezaji huo, ambapo Serikali imepanga kuajiri walimu wastaafu wenye uwezo wa kufundisha waliokuwa wanafundisha masomo ya sayansi kwa mkataba ili kupunguza pengo lililopo.

Aidha, Naibu Waziri Jaffo amebainisha kuwa Serikali inafanya tathimini ya mahitaji ya walimu wa masomo ya sanaa kwa kila Halmashauri ili kubaini maeneo yenye ziada na yenye upungufu ili kusawazisha.

“Mpango wa Serikali uliopo ni kuwahamasisha walimu wa ziada wa masomo ya sanaa kwenda kufundisha katika shule za msingi ndani ya Halmashauri husika, ambapo kabla ya kuanza utekelezaji wa mabadiliko haya Serikali itatoa waraka maalumu kwenda katika Halmashauri zote nchini” amefafanua Naibu Waziri huyo.

Akizungumzia kuhusu utaratibu wa mafunzo ya walimu Mhe. Jaffo amesema kuwa Halmashauri moja haiwezi kuwa na mfumo wa peke yake wa kuandaa walimu hali ambayo iltakuwa ni vigumu kuthibiti ubora wa mafunzo hayo kwa walimu.

Hata hivyo amesema kuwa Serikali itaendelea kuongeza udahili wa walimu wa sayansi katika vyuo vya ualimu kadri watakavyojitokeza ili kukidhi mahitaji yaliyopo 
 

Post a Comment

Toa maoni tu (kejeli na matusi marufuku)

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top