Wanafunzi wahaha Baada ya Serikali Kukifunga Chuo cha Mbeya Polytechnic Kwa Tuhuma za Kudahili Wanafunzi Wasio na Vigezo

Ellertoni Mwamasika (Mkurugenzi wa Chuo cha PolyTechnic)

Baraza la Udhibiti wa Vyuo vya Ufundi nchini Tanzania NACTE imekifungia chuo cha Biashara, Mifugo na Kilimo cha Mbeya Polytechnic kwa kushindwa kukidhi vigezo ikiwa ni pamoja na kudahili wanafunzi wasio na sifa.


Akisoma uamuzi huo kwa niaba ya NACTE, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amosi Makalla amesema kuwa taarifa kutoka NACTE zinaonesha kuwa chuo hichi kina mapungufu mengi ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo ya mifugo ambayo hayajathibitishwa na vyombo husika vya serikali.

Pia amesema kuwa chuo hicho kimekuwa kikidahili wanafunzi wasiokuwa na vigezo, akitolea mfano wanafunzi wanaosoma kozi ya mifugo ambapo kati ya wanafunzi 359 ni wanafunzi 89 pekee ndiyo wanaotambulika kuwa na vigezo husika.


Wakizungumza kwa uchungu baadhi ya wanafunzi wamelalamikia chuo hicho kwa kuwasababishia upotevu wa muda na gharama, ambapo baadhi yao walikuwa tayari wamehitimu na walikwenda chuoni hapo kufuatilia vyeti.


“Mimi nimetoka mbali, nimekuja kufuatilia cheti changu, sasa nina miezi miwili hapa, kila siku nazungushwa nazungushwa, kumbe walijua wanakuja kufungiwa, kwahiyo cheti changu sipati, na muda nimepoteza, nimekaa hapa miaka mitatu halafu leo naambiwa miaka yangu mitatu haina maana tena, sikubali sikubali..” amesema mwanafunzi Catherene Buda

Kwa upande wake Mkurugenzi wa chuo hicho Ellertoni Mwamasika, ameomba radhi na kusema kazi ya kuendesha chuo ni ngumu “Chuo kinawaomba radhi wote, ila mjue kuwa kazi hii ya kuendesha chuo ni ngumu”


Hata hivyo serikali imesema wanafunzi wenye sifa watahamishiwa katika vyuo vingine huku ikimuagiza mmiliki wa chuo hicho kuwalipa wanafunzi gharama zao zote kabla hawajatoka chuoni hapo.
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top