Lipumba kueleza hatima yake ndani ya CUF leo

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, leo anatarajiwa kuzungumza na waandishi wa habari kueleza hatima yake ndani ya chama hicho.


Habari zinasema amechukua hatua hiyo baada ya kuibuika wimbi la wana CUF kumtaka arudi katika nafasi yake ya uenyekiti huku chama hicho kikitangaza kufanyika kwa mkutano mkuu Agosti 21, mwaka huu.


Wakati hayo yakiendelea taarifa za ndani zinaeleza kuwa mwishoni mwa wiki iliyopita Profesa Lipumba, aliondoa barua yake ya kujiuzulu uenyekiti na alikutana na Katibu Mkuu wa CUF na kujadili kwa kina suala hilo.


Chanzo chatu cha uhakika ndani ya CUF kilisema baada ya mazungumzo ya kina, Maalim Seif alimthibitishia Profesa Lipumba, kupokewa kwa barua yake huku akimuomba asubiri ushauri wa wanasheria kuhusu hatima yake ya kurejea ofisini.


“Kesho (leo) Profesa atazungumza na wana habari asubuhi na kikubwa ataeleza kwa kina hatima yake ndani ya CUF.


“Kikubwa tunategemea atafungua ukurasa mpya na kutangaza kukijenga chama chetu,” alisema mtoa habari wetu ambaye yupo karibu na Profesa Lipumba.


Profesa Lipumba alijiuzulu nafasi hiyo Agosti 5, mwaka jana kwa kile alichodai kutoridhishwa na hali ya mambo ikiwamo umoja ndani ya Ukawa na kupokewa kwa aliyekuwa mgombea urais aliyekuwa anaungwa mkono na vyama Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD, Edward Lowassa.


Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na vuguvugu la wana CUF kuendesha makongamano nchi nzima kutaka Profesa Lipumba arudi kwenye madaraka kwa madai kwamba chama hicho kimekosa mtu imara upande wa Bara.


Licha ya hali hiyo wanachama hao walikuwa wakitaka uitishwe Mkutano Mkuu Maalumu ambao unatakiwa kujadili hoja ya kujiuzulu kwa Profesa Lipumba, kwa mujibu wa Katiba ya CUF.
Newer Posts Older Posts
© Copyright UCHAMBUZI LEO | Modified By Smart WEB
Back To Top Back To Top